Zanzibar – Leo, Unguja, Serikali ya Marekani, kupitia mradi wa Afya Endelevu wa Shirika la Marekani la Maendeleo ya Kimataifa (USAID), imesaidia kuajiri wataalamu wa afya 100 kushughulikia mahitaji ya dharura ya UVIKO-19. Wataalamu wa afya watafanya kazi katika maeneo manne ya kuingilia ya bandari na vituo vya afya 33 kwa kutoa huduma za kinga ya UVIKO-19, matibabu na kuharakisha utoaji wa chanjo Unguja na Pemba. Wataalamu hawa wametambuliwa kwa kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na wamepangwa kwenye vituo vilivyo na upungufu mkubwa wa rasilimali watu na maeneo ya kuingilia ya bandari yenye hatari za maambukizi.
Vituo vya afya nchini Tanzania vimekuwa na wafanyakazi wachache, kitu ambacho kinaathiri ubora wa utoaji wa huduma za afya. Wakati janga la UVIKO-19 lilipoikumba Tanzania, upungufu wa wafanyakazi wa afya ulidhihirika zaidi – hasa upungufu wa wafanyakazi wa kusaidia huduma za kinga na matibabu ya UVIKO-19. Kwa kuongezea, kulingana na Ripoti ya Hali ya Serikali ya Septemba 27, 2021, matumizi ya chanjo ya UVIKO-19, yatapunguza sana magonjwa na vifo vinavyohusiana na UVIKO, lakini kiwango cha utoaji wa chanjo bado ni kidogo.
Serikali ya Marekani kwa kushirikiana na Serikali ya Tanzania na Zanzibar zinapunguza athari za janga hilo kwa jamii. Mradi huu unalenga kusaidia upatikanaji na utoaji wa chanjo ya UVIKO-19, kupunguza magonjwa na vifo vitokanavyo na UVIKO-19, kuzuia na kupunguza athari za UVIKO-19 kwenye dharura ya VVU/UKIMWI. Mpaka sasa, USAID iimewekeza kiasi cha Dola za Marekani million 25.1 kwenye maeneo haya.
Ni Muhimu kutambua kwamba Serikali ya Marekani na Wizara ya Afya ya Zanzibar zimeshirikiana kuimarisha uwezo wa wahudumu wa afya na kujenga uelewa katika kuainisha vipaumbele vya afya ya jamii mfano UVIKO-19. Kwa takribani miaka ishirini sasa, USAID imekuwa mstari wa mbele kuendeleza rasilimali watu kwenye sekta ya afya.
Ukitekelezwa kupitia Taasisi ya Benjamin William Mkapa (BMF), mradi wa USAID Afya Endelevu unaimarisha rasilimali watu kwenye afya, eneo ambalo lina rasilimali hafifu nchini Tanzania. Kupitia Afya Endelevu, wataalamu wa afya wameelekezwa kufanya kazi na vituo vya afya teule vinavyokabiliwa na uhaba mkubwa na wameajiriwa katika mchakato wa ushindani ambao unaangalia ustadi na sifa zinazohitajika kukabiliana na changamoto zinazojitokeza za kiafya, kama vile kuonesha mfano katika upataji wa chanjo ya UVIKO-19, na kuboresha ubora wa huduma za kinga na matibabu.
Akizungumza katika hafla hio leo, Mkurugenzi wa Afya wa USAID, Ananthy Thambinayagam alisema “Nguvu kazi na vifaa vya kutosha ni muhimu kwa maendeleo endelevu na utoaji endelevu wa huduma bora za afya na mwitikio dharura kama UVIKO-19. USAID inasaidia uwekezaji katika wafanyakazi wa afya kwa sababu nguvu kazi yenye uwezo inaokoa maisha, haswa sasa katika janga la UVIKO-19”. Ananthy alisisitiza juu ya ufadhili wa USAID kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar tunapoendelea kushirikiana na kudumisha mabadiliko yenye ufanisi zaidi kuelekea kwenye kutoa huduma bora za afya ambazo zinawanufaisha Watanzania wote.